January 21, 2011

Ujerumani yaanzisha kampeni dhidi ya ubaguzi michezoni

Katika kipindi cha hivi karibuni vyama vya siasa kali za mrengo wa kulia pamoja na makundi ya kisiasa yamekuwa yakijiingiza zaidi katika jukwaa la spoti kwa lengo la kutafuta wafuasi na wapiga kura miongoni mwa Wajerumani. Kampeni hiyo dhidi ya siasa kali katika majukwaa ya michezo imezinduliwa mjini Berlin.

Wakati wa msimu wa kandanda nchini Ujerumani viwanja vya Klabu za wachezaji wasiolipwa ambao ni zaidi ya 25,000 nchini hufurika na kujaa msisimko. Ni katika maeneo haya ambapo kila wikiend mamilioni ya mashabiki huteremka na kuja kuonyesha ukereketwa wao katika vilabu vyao vya nyumbani na kuachilia mbali ushabiki wa timu kubwa kubwa za wachezaji wa kulipwa.

Klabu ya Red Star ya mjini Leipzig huko mashariki ya Ujerumani iliyo katika daraja la nane inajivunia kuonyesha alama yake ya nyota nyekundu ambayo inawaashiria mashabiki wake kwamba ni klabu inayoshabikia siasa za mrengo wa kushoto. Hata hivyo katika miezi ya hivi karibuni timu hiyo imejikuta ikilengwa na watu wa siasa za mrengo wa kulia. Na hili limeonekana hasa timu hiyo inapokuwa katika michezo ya mbali na nyumbani ambapo mashabiki wenye itikadi za kibaguzi huwapinga.

Matamshi kama hayo yanayosema kwamba ikiwa huipendi Ujerumani unaweza kuihama au maneno kama Hasta la Vista Antifaschista ikiwa na maana kwamba kwaheri Ufashisti ni baadhi tu ya vibwagizo ambavyo wanakabiliana navyo klabu hiyo inapokuwa mchezoni nje na nyumbani,anasema rais wa Klabu hiyo Sophia Bormann.

Baadhi hutupigia saluti ya Hitler au kutuimbia nyimbo za maneno ya kibaguzi au kutuita majina ya matusi ya kibaguzi kama vile kutuita nguruwe wa ajabu,anasema rais huyo.Katika kijiji cha Mügeln baadhi ya Wanazi mambo leo huwatolea maneno yanayokumbusha ukatili wa utawala wa Wanazi dhidi ya Wayahudi kama vile ''Yahudi aliyetundikwa kwenye mti na kutiwa kitanzi''

Hata hivyo mashabiki wa klabu ya Red Star hawawezi kuwa mashabiki wa kweli ikiwa hawatojibu matusi hayo. Kwa mfano wanawajibu kwa kuwaambia tumewashinda vitani, maneno hayo wanawaambia wanazi mambo leo wanaoshabikia timu nyingine.Malumbano hayo humalizika wakati mechi imekwisha.

Lakini mara nyingi mechi kama hizi humalizikia na fujo na ghasia, kwa mfano mapema katika msimu wa joto uliopita mashabiki wenye kufuata siasa za mrengo wa kulia walivamia uwanjani katika kijiji cha Brandis na kuwavamia mashabiki wa timu ya Red na mitarimbo na kuwajeruhi vibaya watu watatu.

Tukio hilo ni mojawapo ya matukio ambayo yanakumbusha kwamba kuna dosari mahala katika jukwaa la spoti na hasa zinapochezwa mechi za ligi ya chini. Gunther Pilz ni mshauri katika shirikisho la dimba nchini Ujerumani na ameweza kukusanya taarifa za utafiti uliofanywa juu ya kuongezeka kwa ushawishi wa watu wenye siasa kali za mrengo wa kulia katika michezo.

Viongozi wa vyama vya siasa za mrengo wa kulia kama Klaus Beier, mwenyekiti wa chama cha Wanazi mamboleo kinachofuata siasa za mrengo wa kulia, NPD, katika jimbo la Brandenburg anakiri wazi kwamba michezo katika eneo hilo na hasa kandanda,ni jukwaa mwafaka la kueneza fikra za siasa za mrengo huo.

Chanzo:DW-BONN

No comments:

 Wale wajanja wote tunakutana Leverkusen 24.09.22