May 07, 2013

MAMA KIKWETE AKIOMBA KITUO CHA WATOTO WENYE UTINDIO WA UBONGO KUSHIRIKIANA NA TANZANIA KUTOA MAFUNZO KWA WATOTO HAO

FIRST LADY MAMA SALMA KIKWETE

Mke wa Rais Mama Salma Kikwete amekiomba kituo cha watoto wenye mtindio wa Ubongo kilichopo nchini Kuwait kushirikina na Tanzania ili waweze kufanya kazi kwa pamoja ya kuwasaidia na kutoa mafunzo kwa watoto wenye matatizo kama hayo waliopo nchini.

Mama Kikwete alilitoa ombi hilo jana alipotembelea kituo hicho kwa ajili ya kuona jinsi wanavyotoa mafunzo kwa watoto hao ambayo yameweza kuwabadilisha akili zao na kuwa sawa na za watu wengine.
Alisema kuwa watoto wenye mtindio wa ubongo hata nchini wapo na wanapata mafunzo katika vituo vichache zilivyopo lakini kama watashirikiana kwa pamoja wataweza kubadilishana ujuzi ambao utawasaidia kutoa mafunzo mazuri zaidi kwa watoto hao.

“Ninawapongeza kwa kwa kazi kubwa na nzuri mnayoifanya ya kutoa mafunzo kwa watoto hawa kwani ni jambo jema kuwasaidia watu wenye matatizo.

“Watoto hawa wakipewa mafunzo akili yao itakuwa sawa na watu wengine, wakiwa wakubwa na kufikia umri wa kujitegemea wataweza kufanya kazi mbalimbali za maendeleo ambazo zitawaingizia kipato na kuwasaidia katika maisha yao ya baadaye”, alisema Mama Kikwete.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kituo hicho Dk. Samira Al-Saad alisema kuwa kama watoto wenye matatizo ya mtindio wa ubongo watapelekwa shule mapema zinazotoa mafunzo kwa ajili yao watapona na kuwa na akili sawa na watu wengine.
Dk. Samira alisema kuwa wazazi wengi hawajui kwamba matatizo ya mtindio wa ubongo yanatibika kama mtoto akipewa elimu ya darasani na kufanyishwa mazoezi ambayo yatamsaidia kufanya shughuli zake mwenyewe bila ya kutegemea msaada wa jamaa zao.
“Kituo hiki kilifunguliwa mwaka 1994 na hadi sasa kina wanafunzi 120 ambao wanapata mafunzo ya nadharia na vitendo na kinajiendesha kwa kupata msaada kutoa Serikalini, watu na mashirika binafsi ya ndani na nje ya nchi”, alisema Dk. Samira.
Aliendelea kusema kuwa umri wa watoto wa kuanza masomo ni miaka sita hadi 15 na kama mwanafunzi atakuwa amevuka miaka 15 atajifunza zaidi mafunzo ya vitendo ambayo yatamuwezesha kujitegemea hapo baadaye.
Dk. Samira alisema, “Wanafunzi wetu wameweza kupata ajira sehemu mbalimbali hii ni baada ya kupata mafunzo ambayo yamewafanya kuwa na akili sawa na watu wengine ambao hawana matatizo haya, kuna baadhi yao tumewaajiri hapa na hivi sasa wanawafundisha wanafunzi wenzao.
Mama Kikwete pia alitembelea Kituo cha Al-Kharafi ambacho kinatoa huduma ya mazoezi kwa watoto wenye matatizo ya mtindio wa ubungo na kuona jinsi watoto hao wanavyofanya mazoezi yao.

Kituo hicho kinapokea watoto wenye umri wa kuanzia miaka minne hadi 12 ambao wanafanya mazoezi kwa kucheza michezo mbalimbali ambayo inawabadilisha akili zao na kuwa katika hali ya kawaida .

Akiwa katika kituo hicho alijionea kazi mbalimbali zinazofanywa na watoto hao ambazo ni uchoraji, ushonaji, upishi pia aliona michezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na nyimbo na maonyesho ya mavazi.Mama Kikwete aliambatana na Mumewe Rais Jakaya Mrisho Kikwete nchini Kuwait kwa ziara ya kikazi ya siku mbili.

Source:Ikulu

No comments:

 Wale wajanja wote tunakutana Leverkusen 24.09.22