April 16, 2008

Mafisadi

Baada ya kuzua gumzo kutokana na taarifa kuwa ana akaunti yenye mapesa yanayozidi kiasi cha Sh. 1,000,000,000 (Sh. Bilioni Moja) katika benki moja iliyopo katika Kisiwa cha Jersey nchini Uingereza, hatimaye Waziri wa Miundombinu, Bw. Andrew Chenge anatarajiwa kutua nchini na kueleza kila kitu kuhusiana na mapesa hayo. Bw. Chenge anatarajiwa kutoa ufafanuzi mbele ya waandishi wa habari leo, mara baada ya kutua nchini na dege la Emirates, akitokea ziarani nchini India na China alikokuwa ameambatana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bw. Jakaya Kikwete. Habari zilizopatikana Jijini na kisha kukaririwa na kituo cha luninga cha Shirika la Habari nchini, TBC1 zinasema baada ya kuwasili nchini, Waziri Chenge anakusudia kukutana na waandishi wa habari ili kujisafisha tuhuma kadhaa zinazohusiana na habari za mapesa hayo. Tuhuma dhidi ya Waziri Chenge zilianza mwishoni mwa wiki baada ya gazeti la The Guardian la Uingereza kuchapisha habari kuwa Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa ya nchi hiyo, SFO, imegundua akaunti ya Bw. Chenge katika benki moja kisiwani Jersey, ikiwa na pesa za nchi hiyo, Paundi 507.500, ambazo ni sawa na zaidi ya Shilingi Bilioni moja za Kibongo. Kwa mujibu wa gazeti hilo la April 12, fedha hizo zinahisiwa kuwa ni sehemu ya mgao wa rushwa aliyoipata Waziri Chenge kutoka katika kampuni ya BAE System ya nchi hiyo kwa ajili ya kuishawishi Serikali ya Tanzania ili inunue rada kwa bei mbaya ya Paundi Milioni 28 za Uingereza, sawa na karibu Shilingi Bilioni 70 za kibongo. Hata hivyo, gazeti hilo la The Guardian limedai kuwa lililipomhoji Bw. Chenge kuhusiana na fedha hizo, alikiri kuwa kweli ni zake, lakini akakanusha kuwa hazihusiani na sakata la ununuzi wa rada.

No comments:

 Wale wajanja wote tunakutana Leverkusen 24.09.22